Na Ali Issa-Maelezo
Zanzibar
Jumuiya Ya Uamsho Na
Mihadhara Ya Kiislamu (JUMIKI) imepinga uvumi uliosambazwa nchini kuwa leo
kutakuwa na maandamano ya Jumuiya hiyo na kudai kuwa propaganda hizo
zinaendeshwa na baadhi ya watendaji katika jeshi la polisi na usalama wa taifa
ambao hawaitakii mema Jumuiya yao.
Hayo yamesemwa na
Amiri wa Jumuiya hiyo Sheikh Farid Ahmed wakati alipokuwa akizungumza na
Waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Habari Maelezo ZanzĂbar kuhusiana na tuhuma
ambazo wamezitoa kwa Jeshi la Polisi dhidi ya Jumuiya yao.
Amedai kuwa Jumuiya
haijapanga maandamano kwani ni taasisi inayofanya kazi zake kisheria nakwamba
hata ikitokezea kufanya maandamano basi watafuata taratibu zote za kisheria
ikiwa ni pamoja na kulitaarifu rasmi Jeshi la Polisi.
Aidha amedai kuwa kuna
mkakati wa muda mrefu wa kutaka kuwabatiza viongozi wakuu wa jumuiya hiyo kesi
za ugaidi hususan Amir Mkuu wa jumuiya ya Maimamu Zanzibar Sheikh Farid Hadi
Ahmed ili kuzima vuguvugu la kudai Zanzibar huru.
Shekh Faridi amedai
kuwa inasemekana kuna mahusiano makubwa baina ya watendaji ndani ya Jeshi la
polisi pamoja na baadhi ya wageni wanaosadikiwa kuwa ni raia wa Marekani juu ya
kuutekeleza mkakati huo baada ya kuwa tayari umeshakamilika.
Amedai kuwa kuna
ukiukwaji mkubwa wa haki za kirai ambao umekuwa ukifanywa na Jeshi la Polisi
Zanzibar kwa kuwanyima haki ya kufanya mihadhara yao ndani ya Misikiti ambapo
Juni 17 mwaka huu wananchi mbalimbali walijeruhiwa kwa mabomu katika vijiji vya
Donge,Mkwajuni na Mahonda.
Ameliomba Jeshi la
Polisi kufanya kazi zake za kulinda usalama wa wananchi na mali zao na kuacha
kufanya kinyume chake kwani huko ni kuchochea chuki kati ya Jeshi hilo na
raia.
Amesisitiza haja ya
wazanzibari kuungana na kuachana na Itikadi zao za kivyama katika kudai hadhi ya
Rais na mamlaka ya Nchi ya Zanzibar ndani na nje ya Zanzibar pale tume ya
mabadiliko ya Katiba itakapoanza kazi zake.
Kwa upande wake Naibu
Naibu Amir Jumuiya Ya Uamsho Na Mihadhara Ya Kiisilam Sheikh, Azan Khalid Hamdan
amewaomba wanahabari nao kuwa makini katika taaluma yao kwa kufanya usawa wa
taarifa ambazo wamekuwa wakizitoa.
Hivi karibuni Jumuiya
hiyo ilitangaza rasmi kushiriki kikamilifu katika zoezi zima la kutoa maoni yao
katika mchakato wa kupata Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
kubadili msimamo wao wa awali wa kuisusia Tume hiyo.
MWISHO.
IMETOLEWA NA HABARI
MAELEZO ZANZIBAR
26/06/2012